Social Icons

Pages

Thursday, 15 January 2015

KIKOSI BORA CHA MAPINDUZI CUP 2015 ZANZIBAR



Golikipa bora wa michuano ya Mapinduzi, 2015… SAID MOHAMMED- Mtibwa Sugar
Hata kabla hajacheza mkwaju wa penalti wa kiungo Shaaban Kisiga, tayari golikipa wa Mtibwa Sugar, Said Mohammed alionesha kiwango kikubwa katika michezo mitano ya mwisho. Akiwa ameruhusu bao moja tu (sawa na Manyika Peter wa Simba SC), Said alikuwa bora katika uchezaji wa mipira ya krosi na mashambulizi ya moja kwa moja.
Aliibeba timu yake dhidi ya Azam FC katika robo fainali baada ya kucheza mikwaju ya penalti, pia aliisaidia sana timu yake katika nusu fainali dhidi ya Polisi na alikaribia kuwapa taji katika mchezo wa fainali kama si Ibrahim Jeba asingepoteza mkwaju wa penalti wakati Mtibwa wakiwa mbele. Said alistahili hakika kuwa golikipa bora wa michuano…

02; HASSAN KESSY-Simba SC Alitajwa kama mchezaji bora wa mchezo wa mwisho wa hatua ya makundi wakati Simba ilipoicharaza, Taifa ya Jang’ombe kwa mabao 4-0, Kessy amekuwa namba mbili bora katika timu yake licha ya kuichezea michezo tisa tu ta ngu asajiliwe akitokea Mtibwa mwezi Disemba. Aliipandisha timu kwa kasi, alionekana mwenye nguvu kila alipogombania mpira, alipendeza namna alivyomkaba mshambulizi Musa Hassan Mgosi katika michezo miwili waliyokutana katika siku 13 za michuano hiyo.

Katika mchezo wa fainali, Kessy alimzima kabisa Mgosi hadi kupelekea mshambulizi kuoneshwa kadi ya njano. Kwa miaka miwili sasa, Kessy anathibitisha mtazamo wa walio wengi kuwa ndiye mlinzi bora wa kulia kwa sasa nchini. Wakati Shomari Kapombe ameonekana ‘ ku-hodhi’ nafasi ya ‘ beki 2′ katika timu ya Taifa, Taifa Stars mlinzi huyo wa klabu bingwa Bara anatakiwa kuwa makini zaidi na kuzidi kujiimarisha kwani nafasi hiyo iko mbioni kupata ‘ mtu mpya’, wenyewe wanamuita ‘ Dan Alves’ namaanisha Hassan Kessy Ramadhani.

03: MOHAMMED HUSSEIN ‘ TSHABALALA’.- Simba SC
Hili jina la Tshabalala limetokea wapi?. Labda maskani za vijana wa kihuni maeneo ya Magomeni katikati ya jiji la Dar es Salaam, huko unaweza kupata majibu, lakini kwangu linapotamkwa jina hilo namkumbuka mfungaji wa bao la kwanza la fainali za kombe la dunia ‘ WOZA2010′ nchini Afrika Kusini. Huyu alikuwa kiungo mshambulizi akitokea katikati ya uwanja huku akitumia zaidi mguu wa kushoto.
DSC04887
Moja kati ya matukio ya kukumbwa sana katika fainali hizo zilizofana ni bao la Siphiwe Tshabalala dhidi ya Mexico ambalo lilikuwa goli la kuongoza katika mchezo wa ufunguzi ndani ya uwanja wa Soccer City, baada ya mchezo huo jina la Tshabalala likawa juu, huku likitamkwa mara kwa mara na mashabiki wa kandanda barani Afrika. Tumeona mengi kutoka kwa Tshabalala halisi, lakini najiuliza huyo ‘ Tshabalala wa Simba’ amepataje jina hilo. Achana na kuboronga kwa timu hiyo katika ligi kuu, ukirudi katika uhalisia utaungana nami naposema Mohammed Hussein ‘ Tshabalala’ ndiye mchezaji bora wa Simba katika michezo 14 ya ki-mashindano tangu kuanza kwa msimu wa 2014/15.

Anavutia anavyozuia, utapenda kumuona anaposhambulia. Katika mchezo wa fainali aliweza kumdhibiti vilivyo kijana hatari wa ‘ rika lake’, Ally Shomari ambaye amekuwa mchezaji wa hatari katika safu ya mashambulizi ya Mtibwa. Kabla ya michuano hiyo na hata baada ya kucheza michezo miwili ya mwanzo dhidi ya Mtibwa na Mafunzo safu ya ulinzi ya Simba ilionekana ‘ kucheza kwa ku-yumba, yumba’.
Hilo lilichangiwa na namna safu za pembeni katika ‘ fullbacks’ kufanya makosa yasiyo ya lazima. Sasa Simba wamekuwa salama katika michezo mitano mfululizo ambayo wamecheza bila kuruhusu bao, yote imechangiwa na vijana, Kessy katika ‘ beki 2′ na Tshabalala katika ‘ beki 3′. Wanashambulia kwa zamu, mmoja anakwenda, mwingine anabaki kusubiri kucheza ‘ coverage’ inapotekea wameshambuliwa kwa shambulizi la kushtukiza ‘ counter attack’.

04; HASSAN ISIHAKA ‘ Captain mtoto’- Simba SC
Unapokosa timu imara za Taifa katika ngazi ya chini si rahisi kupata mafanikio katika ngazi ya juu kwa kuwa unakwenda kushindana na timu zenye wachezaji waliokomaa kiushindani zaidi yako na wenye uzoefu. Laiti vijana kama, Kessy, Tshabalala, Isihaka wangeendelea kucheza mfululuzo katika michuano ya kimataifa ngazi ya vijana ingewasaidia sana kuwajenga kuelekea timu ya Taifa Stars.

Lakini wataendelea kudumaa katika soka la ndani licha ya kuonesha ukomavu na viwango vya juu katika klabu yao kiasi cha kuaminiwa katika kikosi cha kwanza. Bila shaka umemuona Isihaka, beki wa kati-mtulivu, aliyejipanga na kuwaongoza wenzake muda wote wa michuano. Nyota njema huoneka asubuhi, kijana Isihaka amefuata nyanyo za Shomari Kapombe naye amekuwa ‘ kiongozi, nahodha kijana’ kuiongoza Simba kutwaa taji. Ndiye beki nne bora katika kikosi changu cha michuano.

05; SALIM MBONDE- Mtibwa Sugar
Mtibwa ilimsajilili mlinzi huyo wa kati kutoka timu ya U20 ya JKT Oljoro katikati ya mwaka 2012 na hakuna shaka tena kuwa uamuzi huo uliofanywa na kocha Mecky Mexime umekuwa na ‘ bahati kubwa’ katika soka la Tanzania. Mbonde anawakumbusha watu namna Tanzania ilivyo na vipaji vikubwa. Mtu makini, mtulivu, mwenye busara na mgumu kupitika. Alitajwa kama mchezaji bora wa michuano licha ya timu yake kupoteza mchezo wa fainali.
DSC04804
Alijiamini muda wote alipokuwa na mpira, huku akiwaongoza vijana wenza Ally Lundenga, Vicent Andrew na mzoefu, David Luhende kucheza mchezo wa kutotanuka hata pale Simba waliposhambulia kwa nguvu. Sasa Tanzania inacheka, furaha na kicheko hicho kinaletwa na vipaji timilifu kama cha Mbonde. Kama ukiambiwa uchague wachezaji bora wa safu ya kati katika ngome bila shaka hata ukiwa usingizi utawataja, Isihaka na Mbonde, vijana makini na watulivu.

Wakati wa usajili wa mwezi Agosti kiongozi mmoja wa Simba alimfuata Mbonde na kumwambia ‘ tunataka kukusajili wewe ni sehemu ya mipango yetu’. Mbonde hakupingana naye zaidi akamwambia kiongozi huy wa ‘ mnyama’ aende akazungumze na klabu yake kwa kuwa bado ana mkataba wa miaka miwili. Kila kitu kilikwama baada ya kiongozi huyo kumwambia mchezaji akavunje mkataba wake na Mtibwa wao wataingia kumalizia mchakato wa usajili jambo ambalo Mbonde alilikataa na kulifikisha kwa uongozi wake. Wangejua…, itapendeza siku Isihaka akihamia Mtibwa ili akacheze na Salim, au Mbonde kuhamia Simba siku akacheze na Isihaka katika ngome ya kati.

06; JONAS MKUDE.-Simba SC
Katika nafasi hii kuna wachezaji kadhaa wamefanya vizuri, Mudathir Yahya wa klabu ya Azam FC, Salum Telela wa Yanga SC lakini nilihitaji mchezaji bora zaidi na bila wasiwasi nitampanga Mkude, kiungo wa ulinzi wa Simba SC ambaye alicheza kwa kiwango kilekile tu. Nahodha wa Mtibwa, Shaaban Nditti alicheza kwa kiwango cha juu katika mchezo wa fainali, hata Henry Joseph pia ameweza kucheza vizuri . Mkude anapanga mshambulizi vizuri, anashambulia na kuzuia kwa wakati husika hana cha kutuonesha zaidi ya kuendelea kujitunza kwa kuwa hana mpinzani katika nafasi hiyo, huyu pia ni kijana aliye chini ya U21.

07; SAIMON MSUVA.-Yanga SC
Wala huitaji kuumiza kichwa ili kumpata mchezaji wa nafasi hii, unapoona kiungo wa kulia akifunga mabao manne katika michezo minne bila shaka unashawikika kuamini ni mchezaji bora. Licha ya Yanga kuondolewa katika robo fainali, Msuva amefanikiwa kutwaa tuzo ya mfungaji bora wa michuano. Uchezaji wake wa kasi, ujanja na mbinu za kufunga mabao yasiyotarajiwa vinamfanya nimuweke katika kikosi change bora cha michuano. Ni winga wa kizamini ambaye anaweza kucheza katika mfumo wowote wa kisasa na kutoa matunda.

08; MUDHAMIR YASINN- Mtibwa Sugar
Alicheza kwa kiwango cha juu dhidi ya Azam FC katika robo fainali, akafanya hivyo tena katika mchezo wa nusu fainali dhidi ya JKU, na namna alivyocheza dhidi ya Simba SC katika mchezo wa fainali nimeshawika kumpanga mchezaji huyo chipukizi katika nafasi ya kiungo wa mashambulizi. Licha ya Mtibwa kufunga mabao matatu tu katika michezo sita ya michuano hiyo, Yassin aliweza kuifanya timu hiyo kuwa ngumu kupitika katikati ya uwanja.
Akishirikiana na Nditti na Mussa Nampaka mchezaji huyo ameonekana kucheza kwa kujiamini mno huku akipanga mashambulizi na kupiga pasi za uhakika kwa washambuliaji wake. Alikimbia pale timu ilipokuwa katika spidi, na alipoa huku akitafakari namna ya kupora mipira. Akicheza na Mkude katikati ya uwanja itakuwa ‘ balaa’.

09; KPAH SHERMAN-Yanga SC
Ni mshambulizi pekee wa kati aliyeonesha kiwango kizuri katika michuano hiyo. Mliberia huyo anaingia katika kikosi change bora ikiwa amefunga mabao mawili katika michezo minne aliyocheza. Alionesha mwenye uwezo wa kumiliki mpira, kujipanga na umaliaji wa kiwango cha mchezaji wa kimataifa. Anaingia katika kikosi hiki kama mshambulizi wa kwanza.

10; DANNY SSERUNKUMA-Simba SC
Ni wachezaji wawili tu wa kigeni ambao wamepata nafasi katika kikosi hiki, baada ya Sherman wa Yanga SC, Mganda, Danny Sserunkuma pia anaingia kama mshambulizi wa pili. Danny hajafunga bao katika michuano hiyo lakini namna alivyokuwa akijipanga, kutoa pasi, kumiliki mpira na utoaji wa pasi kwa wenzake ndiko kumechangia kwa kiasi kikubwa safu ya mashambulizi ya Simba kuwa na kasi. Ni mshambuaji bora wa pili katika michuano ambaye alimiza majukumu yake vizuri, ndiye aliyepiga penalti ya mwisho ya Simba kabla ya golikipa Ivo Mapunda kucheza mkwaju wa Vicent Barnabas na kuipa taji timu yake.

11; RAMADHANI SINGANO-Simba SC
Singano alikwenda Zanzibar akishutumiwa kushuka kwa kiwango chake, lakini michuano ya Mapinduzi imeweza kuwaonesha watu namna mcheaji huyo wa kiungo akitokea pembeni ya uwanja alivyo mkali. Alikuwa na kasi, ufundi huku bao lake la mkwaju uliokufa dhidi ya JKU katika mchezo wa nusu fainali likibaki kuwa miongoni mwa mabao bora zaidi katika michuano. Alikuwa mkali na alifanikiwa kufunga mabao mawili. Andrey Coutinho wa Yanga pia alifanya vizuri katika michuano hiyo ikiwemo kufunga mabao matatu katika michezo minne ila nampanga Singano katika nafasi hii kwa kuwa ametuonesha kuwa tulikosea kumsema, ameanza kuchuja.
 
FULU VIWANJA