Social Icons

Pages

Tuesday, 17 December 2013

GENNARO GATTUSO AKANUSHA TUHUMA ZA KUPANGA MATOKEO MECHI

KIUNGO wa zamani Mpiganaji na Mahiri wa Italy na AC Milan Gennaro Gattuso amekanusha vikali tuhuma za kuhusika na upangaji matokeo Mechi kiasi cha kudai kuwa endapo atapatikana na hatia atajiua.
Gattuso, ambae Mwaka wa 2006 alitwaa Kombe la Dunia akiwa na Italy, mapema Jumanne alitajwa na Vyombo vya Habari vya Italy kuwa anahusika kwenye tuhuma za upangaji matokeo Mechi na yupo kwenye uchunguzi unaoendeshwa na Mwendesha Mashitaka wa Ofisi ya huko Cremona.
Pamoja na Gattuso pia yupo Kiungo wa zamani wa Lazio Cristian Brocchi na wote wanahusishwa na tuhuma kuwa walikula njama katika Msimu wa 2010/11 kupanga Matokeo ya Mechi za Serie A na nyinginezo.
Inadaiwa Gatusso na Brocchi walikuwa na uhusiano kwa Simu na Watu wanne ambao wamekamatwa na Polisi kwa madai hayo ya kupanga Matokeo Mechi.
Mara baada ya kuibuka tuhuma hizo, Gattuso alikaririwa kwenye Sky Sport Italia akisema: “Sijawahi hata Siku moja kuwa na fikra ya kupanga Matokeo Mechi. Kama watathibitisha niko tayari kwenda Mtaani, na najua hiki ni kitu kizito kusema, nitajiua mwenyewe.”
Aliongeza: “Yeyote anaenijua mimi anajua sikubali kufungwa hata Mazoezini, na hata kwenye Mchezo wa Karata na Rafiki zangu. Nimekasirika na nimedhalilishwa. Nataka kujisafisha nisiwe na doa kwenye maisha yangu ya Soka. Sijacheza Kamari maishani mwangu!”
Gattuso, mwenye Miaka 35, alistaafu kucheza Soka mapema Mwaka huu na kuingia kwenye Ukocha lakini amekuwa hana kazi tangu atimuliwe kuifundisha Palermo, inayocheza Serie B, Mwezi Septemba.
Brocchi ni Kocha wa Timu ya Vijana ya AC Milan.
 
FULU VIWANJA