Social Icons

Pages

Thursday, 5 December 2013

BIN KLEB,ASEMA NI NGUMU KUMSAJILI OKWI

MWENYEKITI wa Kamati ya Usajili ya Yanga SC, Abdallah Ahmed Bin Kleb amesema kwamba ni vigumu kwao kumsajili mshambuliji Emmanuel Okwi wa Uganda kwa sababu ya sakata lake na klabu yake ya zamani Simba SC.  Na kuhusu Dan Sserunkuma, Bin Kleb amesema mchezaji huyo aling’ara katika mechi moja ya Kombe la Mataifa ya Afrika Mashariki na Kati, CECAFA Challenge dhidi ya timu dhaifu, Eritrea nchini Kenya, hivyo hawajajiridhisha juu ya ubora wake. “Katika mechi na Eritrea Sserunkuma alitoa pasi za mabao yote na akasababisha penalti ya bao lingine, Uganda ikashinda 3-0. Lakini ni mapema sana kumfikiria kumsajili, labda tumuone kwenye hatua zijazo akiendelea kufanya vizuri, tutamfikiria, ila kwa sasa hatujafanya lolote,”alisema Bin Kleb. Kleb alisema jana alikuwa kwenye mazoezi ya timu yao, Yanga Uwanja wa Bora Kijitonyama, Dar es Salaam na akajionea namna wachezaji wao wanavyojituma mazoezini na kuonyesha ubora wao. “Tulikuwepo Kamati nzima ua Usajili, mimi Seif Magari, Mussa Katabro na Isaac Chanji, kwa kweli wachezaji wote wanajituma sana, huu ni mtihani, kweli tunahitaji kuongeza mshambuliaji mmoja kwa ajili ya michuano ya Afrika, lakini awe mshambuliaji kweli, kuliko kujaza nafasi tu, tuko makini mno katika hilo,”alisema. Kuhusu Okwi, Kleb alisema ni vigumu mno kumsajili kutokana na sakata la klabu yake zamani, Simba SC na Etoile du Sahel ya Tunisia. “Huyo mchezaji (Okwi) kwa kweli ile hata kurudi kucheza Uganda (SC Villa) ilikuwa bahati sana, sakata lake ni zito sana, lazima kwanza Simba SC walipwe fedha zao (dola za Kimarekani 300,000),”alisema. Pamoja na hayo, Bin Kleb amesema anaridhishwa na viwango vya wachezaji wao waliopo Challenge katika timu mbalimbali. Katika kikosi cha Rwanda, Yanga inaye Haruna Niyonzima, Uganda Hamisi Kiiza na Tanzania Bara Deo Munishi ‘Dida’, Kevin Yondan, Frank Domayo, Athumani Iddi ‘Chuji’, Hassan Dilunga na Mrisho Ngassa. 
 
FULU VIWANJA